Mcheza filamu Marekani kuja nchini |
Calvin Kiwia MCHEZA filamu mahiri wa Marekani, Deidre Lorenz atashuhudia pambano la kimataifa lisilo na ubingwa kati ya Rashid “Snake Man” Matumla na bondia toka Russia 'The Rumble on the Mountain' utakaofanyika Moshi Juni 22, mwaka huu. Akizungumzia ujio nyota huyo jana, Rais wa Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBC), Onesmo Ngowi alisema, Lorenz anayeishi New York, atawasili nchi hivi karibuni kwa ajili ya kushiriki kwenye mbio za Marie Frances Mt.Kilimanjaro Marathon kwa kumbukumbu ya miaka 50 ya Uhuru wa Tanganyika. Alisema mbio hizo zitafanyika kwenye mji wa Moshi Juni 24, mwaka huu zikianzia Moshi Club hadi Mamboleo madukani kupitia mzunguko wa YMCA. Lorenz ambaye amecheza sinema nyingi ikiwemo sinema yake iliyompatia umaarufu mkubwa ya Santorini Blue iliyoiuzwa kwa zaidi ya dola za Kimarekani miloni 100, atapata pia fursa ya kushuhudia pambano hilo la masumbwi. Alisema ujio wa mcheza sinema huyo unadhihirisha jinsi Tanzania hususani mlima Kilimanjaro unavyowavutia watalii wengi toka pande mbalimbali duniani. Alisema pia, kutakuweko na mapambano ya utangulizi yatakayowashirikisha mabondia wa Tanzania, Kenya na Uganda. Pascal Bruno wa Tanzania atazichapa dhidi ya James Kitasi wa Kenya, Alibaba Ramadhani dhidi ya Sebyala Med wa Uganda, Allen Kamote dhidi ya Charles Damas, Simom Bernard dhidi ya Saidi Yazidu. "Ujio wa Lorenz ni moja ya mikakati ya TPBC ikishirikiana na mashirikisho ya ngumi duniani kama IBF na CBC pamoja na majiji kadhaa hapa nchini kukuza ajira kwa vijana, kukuza utalii wa michezo (Sports Tourism) pamoja na kujenga mazingira mazuri kwa wawekezaji kuwekeza hapa Tanzania," alisisitiza Ngowi. Baadhi ya sinema alizowahi kucheza Lorenz ni pamoja na: Santorini Blue, The Great Fight, The Emperor's Club, Le viager (2007), Focus Room (2003), Law & Order, Special Victims Unit, Baggage, August Rush, Perfect Stranger, BelzerVizion, Copy That, El Cantante na Two Weeks Notice. Chanzo: Mwananchi Communications Ltd |