For home theatre system solution

Friday, March 30, 2012

Waziri matatani Arumeru  Send to a friend
Thursday, 29 March 2012 23:04
0digg
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Nape Nnauye (kushoto) akimnadi mgombea wa ubunge wa chama hicho katika kampeni za uchaguzi mdogo wa jimbo la Arumeru Mashariki, Sioi Sumari (katikati) kwenye mkutano uliofanyika katika kijiji cha Ambureni jana. Picha na Edwin Mjwahuzi.
VIJANA WA CHADEMA WAMZINGIRA , AHOJIWA NA POLISI
Waandishi Wetu, Arumeru
NAIBU Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Goodlucky Ole Medeye juzi usiku aliingia matatani baada ya kutiwa msukosuko na vijana wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), wakimtuhumu kujihusisha na utoaji rushwa kwenye kampeni za uchaguzi mdogo wa ubunge zinazoendelea Jimbo la Arumeru Mashariki.

Tukio hilo, lilitokea kati ya saa 12:30 jioni na saa 1.20 usiku eneo la Kata ya Mbuguni wilayani Arumeru, pale Naibu Waziri huyo alipokurupushwa na vijana hao, kisha kukimbilia Shule ya Msingi Oldevesi, kabla ya kuokolewa na polisi.

Taarifa kwamba Medeye amekamatwa, zilisambaa kwa kasi hali iliyosababisha watu kadhaa kwenda Kituo cha Polisi Usa River kupata taarifa kamili za tukio hilo, lakini ilifahamika kuwa, Naibu waziri huyo hakufikishwa polisi baada ya kutolewa Mbuguni.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Thobias Andengenye akizungumza na Mwananchi kwa simu jana, alisema walipata taarifa kutoka kwa vijana hao juzi kwamba Naibu Waziri huyo alikuwa anafanya kampeni eneo la Shambarai.

Gazeti hili lilipomtafuta Naibu waziri huyo kupata ukweli wa tukio hilo,  alikiri kukumbwa na mkasa huo, lakini alikanusha madai kwamba alikuwa akigawa fedha kwa lengo la kukisaidia Chama Cha Mapinduzi(CCM).

Hata hivyo, habari kutoka Mbuguni zilizolifikia Mwananchi, zilidai kuwa Medeye ambaye pia ni Mbunge wa Arumeru Magharibi, alikutwa na mkasa huo alipokuwa kwenye mazungumzo na mmoja wa wamiliki wa mashamba makubwa katika eneo hilo, mwenye asili ya kiasia (jina tunalihifadhi), pamoja na wanawake kadhaa ambao ni wakazi wa kata hiyo.

Baadhi ya vijana wanaodaiwa kuwa wafuasi wa Chadema, walimzingira Medeye na kuanza kumhoji sababu za kuwepo eneo hilo  na kugawa fedha kwa lengo la kukisaidia CCM huku akitumia gari la Serikali, hali iliyozua tafrani na kusababisha Naibu Waziri huyo kutimua mbio hadi Shule ya Msingi Oldeves.

Wakati wakiendelea kujibizana, mmoja wa vijana hao alimpiga picha Naibu Waziri huyo pamoja na gari hilo lililokuwa na bendera ya taifa, na kwamba kitendo hicho kilimkera kiongozi huyo kiasi cha kutaka kuvunja kamera, hatua iliyochangia kuongeza kwa tafrani hiyo.

“Baada ya hali ya hewa kuchafuka, baadhi ya wakereketwa wa CCM walipiga simu Kituo cha Polisi Mbuguni, askari wakafika mara moja na kuondoka na Medeye hadi Kituo cha Polisi Mbuguni," alidai mmoja kati ya mashuhuda wa tukio hilo.

Thursday, March 22, 2012

MALI

Wanajeshi watangaza mapinduzi Mali

 22 Machi, 2012 - Saa 09:07 GMT

Wanajeshi waasi wametangaza katika televisheni ya taifa ya
Mali kuwa wamechukua udhibiti wa nchi, saa kadha baada ya kuvamia kasri ya rais.
Wanajeshi walioasi wanasema kuna marufuku ya kutotoka nje katika nchi nzima na kwamba katiba haitatumika kwa sasa.
Bamako
Marufuku kutoka nje nchini Mali
Siku ya Jumatano wanajeshi hao walifyatuliana risasi na wanajeshi watiifu kwa serikali.
Wanasema serikali haijawapa silaha za kutosha kukabiliana na waasi wa jamii ya Tuareg.
Tayari walikuwa wamechukua udhibiti wa kituo cha taifa cha redio na televisheni na kusitisha matangazo.

Baada ya saa kadha ya kuonyesha picha za nyimbo za wanamuziki wa Mali, kundi la wanajeshi likaonekana kwenye televisheni mapema siku ya Alhamisi, wakitambulishwa kama "Kamati itakayorudisha Demokrasia na kutuliza hali katika nchi".

Msemaji wa waasi hao, aliyetajwa kwa jina la Luteni Amadou Konare, alisema sasa wamemaliza "utawala usio thabiti" wa Rais Amadou Toumani Toure.

LUDEWA

  •  HATIMAYE DIWANI ALIYEJINYONGA LUDEWA AZIKWA
    Na Godlove Mtokambali
    Mheshimiwa diwani Rudolf Chaula ambaye alijinyonga ofisini kwake amezikwa jana tarehe 22/03/2012 katika makaburi ya kanisa katoliki kata ya mlangali. 
     
    Umati mkubwa sana ulifurika kumsindikiza marehemu katika makazi yake ya mwisho, ukiwemo uongozi wa wilaya ya Ludewa na madiwani wa kata mbali za Ludewa. 
     
    Inasadikika kwamba marehemu alijinyonga baada ya kudhukumiwa kiasi cha shilingi milioni 81.
     
    Mwendesha msiba alisoma kikaratasi alichokiacha marehemu ambacho kinadai kati ya shilingi milioni 81 alizodhulumiwa, milioni 41 zilikuwa ni mali ya SACCOS Mlangali na milioni 40 ni mali ya familia ya marehemu. 
     
    Uongozi wa kanisa katoliki uligoma katakata kuuombea mwili wa marehemu. 
     
    Marehemu alijinyonga usiku wa kuamkia majuzi katika mojawapo ya vyumba anavyotumia kama ofisi yake ya udiwani kwa kamba ya mbuzi.

Monday, March 19, 2012

DIWANI WA CCM LUDEWA AJINYONGA USIKU HUU

Marehemu Rudolph Chaula a.k.a Kacheche kushoto

Chama cha mapinduzi (CCM) wilaya ya Ludewa mkoa mpya wa Njombe kimepata pigo kubwa kufuatia diwani wake wa kata ya Mlangali Rudolph Chaula maaarufu kwa jina la Kacheche kujinyonga .

Taarifa ambazo mtandao huu wa www.francisgodwin.blogspot.com umezipata hivi na kuthibitishwa na katibu wa CCM wilaya ya Ludewa Eva Degeleki zinadai kuwa diwani huyo amekutwa akiwa kajinyonga katika moja kati ya vyumba vya nyumba yake ambavyo katika enzi ya uhai wake alikuwa akitumia kama ofisi yake ya udiwani.

Katibu huyo wa CCM Ludewa amesema kuwa hadi sasa hana taarifa za chanzo cha kifo chake ila anataarifa ya kujinyonga kwa diwani huyo na kuwa amepokea taarifa hiyo mida ya saa 8.15 usiku huu kujulishwa juu ya kifo hicho.


Imedaiwa kuwa diwani huyo toka mida ya mchana familia yake ilikuwa ikimsaka bila mafanikio baada ya wageni kufika kumuulizia na jitihada za kutafuta huku na kule zilimezao matunda usiku huu baada ya kuwa na wazo la kuvunja chumba hicho na kumkuta diwani huyo akiwa kajinyonga.
 

Habari kwa hisani ya: www.francisgodwin.blogspot.com 

Hali ya Muamba yaimarika.

Kiungo wa timu ya Bolton Wonderers Fabrice Muamba
football365.com

Na Sabina Chrispine Nabigambo
Hali ya kiungo wa timu ya Bolton Wanderers Fabrice Muamba imeripotiwa kuwa imara baada ya kuanguka na kupoteza fahamu hapo jana wakati wa mchezo wa robo fainali ya kombe la FA baina ya timu yake na Tottenham.

Muamba aliripotiwa kupoteza fahamu baada ya kuanguka akiwa peke yake katika dimba la White Hart Lane na kupelekwa katika hospitali ya Chest ya jijini London ambako anapatiwa matibabu chini ya uangalizi maalum.
Kufuatia tukio hilo muda mfupi baadaye mchezo huo ulisitishwa huku timu zote zikiwa zimetoshana nguvu ya bao moja kwa moja.
Taarifa kutoka vyanzo vya hospitali ya Chest zinaeleza kuwa hali ya Muamba inazidi kuimarika.
Dk Slaa afunika kampeni Arumeru             
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa akimnadi kwa wananchi mgombea Ubunge Jimbo la Arumeru Mashariki kwa tiketi ya chama hicho, Joshua Nassari katika mkutano wa kampeni uliofanyika jana kwenye Uwanja wa Soko la Tengeru kwa Pole, kijiji cha Nguruma, Kata ya Akheli, Picha na Edwin Mjwahuzi

KATIBU Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa jana alitua Arumeru Mashariki na kuhutubia mkutano uliotikisa eneo la Kwapole – Soko la Ndizi, huku wazazi wa mgombea wa chama hicho, Joshua Nassari wakipanda jukwaani kujibu matamshi yaliyotolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Steven Wassira dhidi ya mtoto wao.

Mchungaji Samuel Nassari na mkewe, waliwaambia mamia ya watu waliofika kwenye uwanja huo kuwa walitoa baraka kwa Joshua kugombea nafasi hiyo wakisema mtoto wao ni mwadilifu anayefaa kuwawakilisha wananchi wa Arumeru Mashariki bungeni.

Kauli ya Mchungaji Nassari inatokana na matamshi ambayo yamekuwa yakitolewa na Wassira katika kampeni za kumnadi mgombea wa CCM, Sioi Sumari kwamba mgombea wa Chadema hana nidhamu na kwamba amewachosha wazazi wake kwa kutokuwa na nidhamu.

Lakini jana, baba wa mgombea huyo akiwa na mkewe jukwaani alisema: “Mimi siyo mwanasiasa, lakini nimelazimika kupanda jukwaani leo kutokana na matamshi yaliyotolewa na Wassira, napenda kusema hivi Joshua alipata baraka za familia.”

Alisema kabla ya kugombea, Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alifika nyumbani kwake Songoro na kuwaeleza kuwa wanamtaka Nassari kugombea tena na kusema kwamba familia ilikubali na kumpa baraka zote ikiwa ni pamoja na kuwaita wachungaji kumwombea.

Mchungaji Nassari pia alikanusha madai kwamba mwanaye alikuwa jeuri tangu shule akisema hajawahi kufukuzwa wala kusimamishwa masomo kwa utovu wa nidhamu tangu akiwa shule ya msingi hadi alipohitimu masomo ya shahada, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Mchungaji huyo alisema, mtoto wake alisoma katika shule ya msingi, Sekondari ya Bagamoyo kidato cha kwanza hadi cha nne na Shule ya Sekondari ya Wavulana Tabora kidato cha tano na sita.

“Alipokuwa chuo kikuu, ninatambua kwamba alikuwa mtetezi wa wenzake, hivyo ndugu zangu Joshua Nassari anafaa kuwa mbunge na suala kuwa hajaoa halina msingi kwani mke bora mtu anapewa na Mungu na siyo utashi wake au hamu yake, kwani mke siyo kitunguu cha kununua sokoni,” alisema Mchungaji Nassari.

Mapokezi ya Dk Slaa
Dk Slaa ambaye alihutubia mkutano wa kampeni kwa mara ya kwanza katika uchaguzi huo mdogo, alilakiwa na mamia ya watu na magari ulianzia Uwanja wa Ndege ya Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) hadi eneo la Kwapori, Kata ya Akheri ambako mkutano huo ulifanyika.

Msafara wa kumsindikiza Dk Slaa kuelekea Uwanja wa Kwapori ulianza mara tu baada ya kuwasili KIA majira ya saa tisa alasiri. Msafara huo uliokuwa umesheheni magari na pikipiki, ulifunga kwa muda Barabara ya Arusha-Moshi katika eneo hilo.

Akihutubia mkutano huo, Dk Slaa alisema Chadema kinataka wakazi wa Jimbo la Arumeru Mashariki, kumchagua Nassari si kwa sababu ana sura nzuri, bali wanataka kumtuma katika Halmashauri ya Meru na bungeni.

“Halmashauri ya Meru ina tatizo kubwa la ubadhirifu wa fedha za umma, fedha za afya, elimu na barabara zinaliwa na hili nina ushahidi nalo kwa sababu nilikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), kwa hiyo Nassari anatakiwa kwenda kufanya kazi ya kudhibiti wizi huo,” alisema Dk Slaa na kuongeza:

“Hata huko bungeni hatumtumi kwenda kufanya kazi ya Chadema wala Mbowe (Freeman) hapana, hatumtumi kwenda kusinzia wala kuzomea, anatakiwa kwenda kufanya kazi ya watu wa Arumeru ambayo kwa miaka 50 ya Uhuru CCM wameshindwa kuifanya.”

Alisema alipokuwa Mwenyekiti wa LAAC alibaini ubadhirifu wa kutisha katika Halmashauri ya Arumeru wakati huo na hadi sasa unaendelea.

“Kuna wizi mkubwa, fedha za barabara, fedha za maji, fedha na elimu, zimeliwa na hii ni kwa kuwa hakuna mbunge au diwani wa Chadema katika Halmashauri ya Meru,” alisema Dk Slaa.

Alisema wanataka Nassari awe mtetezi wa haki za Jimbo la Meru bungeni kwani wabunge wa CCM kamwe hawawezi kuisema Serikali yao bungeni.

Ujumbe wa polisi
Akizungumza katika mkutano huo, Dk Slaa alisema polisi ambao wametumwa kusimamia amani katika jimbo hilo wamemtumia ujumbe wakilalamikia kulipwa posho ya Sh10,000 kwa siku ambayo haikidhi mahitaji yao.

Dk Slaa alimwomba Nassari kuwasaidia polisi hao kwa kutetea maslahi na stahili zao pindi atakapochaguliwa kuwa mbunge.

“Wamenitumia ujumbe polisi, walimu na wafanyakazi wengine, wanajua watetezi wao ni wabunge wa upinzani, hivyo nawaomba wakazi wa Meru kumchagua Nassari ili aende kuwatetea,” alisema Dk Slaa.

Aliwaomba wakazi wa jimbo hilo, kuendelea kumchangia Nassari ili aendelee na kampeni kwani hana fedha tofauti na mgombea wa CCM.

Kuhusu tuhuma alizotoa Wassira dhidi yake, kwamba yeye (Dk Slaa) alifukuzwa upadri kutokana na kula fedha za ujio wa Papa na kuwa bado anatafutwa, alisema waziri huyo ni mwongo na hajui asemalo. Alisema ikiwa tangu mwaka 1991 bado hajakamatwa, basi Serikali iliyopo madarakani inalea wezi.

Alisema Papa alifika nchini tangu mwaka 1991 na tangu wakati huo yeye yupo nchini na hajawahi kuulizwa kama alikula fedha au kutafutwa akisema kama ni kweli anatafutwa kwa miaka yote hiyo, basi Serikali ijiuzulu kwa kushindwa kumkamata.

“Kama tangu mwaka 1991 nipo, basi kitendo cha Serikali kushindwa kunifungulia mashtaka ya wizi wa hizo fedha basi ni Serikali dhaifu na ijiuzulu,” alisema Dk Slaa.

Lema amuonya Lowassa
Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema amemuonya Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa kutofika Arumeru akisema akifanya hivyo, wataweka hadharani kashfa zote zinazomkabili.

“Tumesikia anakuja Arumeru, tunamkaribisha lakini tunamwonya maana tutamshughulikia ipasavyo, tunafahamu mengi sana kuhusu tuhuma zinazomkabili, akithubutu kukanyaga hapa basi imekula kwake,” alisema Lema.

Kwa upande wake, Nassari alisema: “Mimi siombi ubunge kwa ajili ya kutafuta utajiri kama wengine wanavyofanya, ninatambua tabu zetu Arumeru, kina mama wanavyobeba bidhaa zao na kuingiza sokoni lakini wanatozwa ushuru mkubwa, haya yote ni mambo muhimu ya kushughulikia.”

“Masoko mengi tunayo tangu enzi za utoto wetu, licha ya kwamba wanatoza ushuru lakini miaka yote mnafanya biashara kwenye mvua na jua. Nipeni nafasi tufanye kazi pamoja ya kukabiliana na matatizo haya.”

Chadema washambulia waandishi

Wafuasi wanaosadikiwa kuwa ni wa Chadema jana walifunga Barabara ya Moshi-Arusha eneo la Maji ya Chai na kulishambulia gari lililokuwa limebeba waandishi wa habari waliokuwa katika msafara wa CCM uliokuwa ukipita katika barabara hiyo ukitokea Kata ya Leguruki.

Wafuasi hao walilirushia mawe gari hilo na kulipasua kioo cha nyuma na kumjeruhi Mwandishi wa Habari wa Gazeti la Mtanzania, Eliya Mbonea.

Muda mfupi baadaye, polisi walifika katika eneo hilo na kuwatawanya wafuasi hao.

Mlezi wa chama hicho mkoani Arusha, Steven Wassira alilaani kitendo hicho akisema hakivumiliki na kuvitaka vyombo vya sheria kuchukua mkondo wake.

Katika hatua nyingine: Gari linalodaiwa kuwa la wafuasi wa Chadema, jana lilivamia mkutano wa CCM katika Kata ya Leguruki na kutimua vumbi uwanjani hapo kwa muda kabla ya kuondoka na kutokomea kusikojulikana.
Imeandikwa na Neville Meena, Mussa Juma na Moses Mashalla.
   

WAZIRI MAIGE AFICHWA UKWELI NJOMBE AGEUKA MBOGO

Waziri wa maliasili na utalii Mhe. Ezekiel Maige ameingiwa na hofu juu ya ujenzi wa nyumba mbili katika eneo la Wanging'ombe Wilaya ya Wanging'ombe mkoa wa Njombe baada ya kutembezwa kutazama nyumba hizo bila kusomewa taarifa ya mradi mzima .

Waziri Maige ambaye ametembelea ujenzi wa nyumba hizo jioni hii ameonyesha wasiwasi wake wa kubebeshwa maji katika tenga ( kudanganywa ) baada ya kukagua nyumba hizo ambazo mradi wake ulianzwa kutekelezwa mwaka 2004 bila ya kukamilika hadi sasa.

Baada ya kukagua mradi huo waziri Maige aliomba kusomewa taarifa ya mradi huo bila mafanikio zaidi msimamizi wa mradi huo ambaye ni meneja wa pori la akiba la mpanga Kipengele Bw.Benison Kibonde kudai kuwa taarifa ya mradi huo ameisahau ofisini kwake.

Kutokana na kukosekana kwa taarifa rasimi ya ujenzi huo jopo la wanahabari lilimvaa waziri huyo na kuomba kusaidiwa kupewa taarifa hiyo bila mafanikio zaidi ya meneja wa mradi huo kuishia kuomba kupewa mud a wa kutafuta taarifa hiyo.

Wanahabari hao walifikia hatua ya kuhoji zaidi juu ya ujenzi huo baada ya kuona sehemu ya jengo hilo likivunjwa jambo ambalo waliomba kuonyeshwa BOQ ya ujenzi huo na kujua gharama za marekebisho ya majengo hayo inatoka katika mfuko gani wakati tayari serikali ilitenga bajeti husika.

Kutokana na maswali hayo ya wanahabari meneja wa mradi huo alimweleza waziri kuwa gharama za ukarabati wa majengo hayo inachukuliwa na mkandarasi husika .

Akitolea ufafanuzi juu ya hoja za wanahabari hao waziri Maige alisema kuwa maswali ya wanahabari hao yamemgusa na hivyo kumwagiza meneja wa mradi huo kuhakikisha anawasilisha taarifa hiyo Leo kabla ya kuondoka mkoani Njombe Kwenda mkoa wa IRINGA .

wakati huo huo watumishi wa idara hiyo wameeleza changamoto mbali mbali zinazowakabili zikiwemo za kutojua mipaka ya hifadhi hiyo kutokana na mwingiliano uliopo Kati ya wananchi na eneo la hifadhi.

Pia suala la Kupanda kwa mishahara yao huku wakimpongeza meneja wao Benison Kibonde kwa kazi nzuri ya kusimamia ofisi hiyo kutokana na meneja aliyekuwepo Awali kutokuwa na mahusiano mazuri na watumishi wenzake.

wakati huo huo waziri Maige amesema kuwa meneja huyo hajamtendea haki kutokana na kushindwa kutoa taarifa ya mradi wa ujenzi wa nyumba pamoja na taarifa nzima ya ofisi yake na kuwa kutofanya hivyo ni kutomtendea haki.


"Kwa kweli kupewa taarifa ya mdomo bila kusomewa wala kupewa nakala ya taarifa husika ni kutonitendea haki Kwani taarifa Ndio inanifanya kuweza kujua zaidi na Kwenda kuitendea kazi.....sasa kushindwa kunipa taarifa ni kutonitendea haki Kabisa ...japo nimeagiza kupewa taarifa hiyo nikiwa Makambako ila bado ni kutonitendea haki kutokana na wakati huo Mimi ni wakati wa kupumzika"

Katika hatua nyingine Waziri Maige amewataka askari hao kufanya kazi kwa kuzingatia maadili na sheri a badala ya kuendelea kuwabambikizia wananchi makos a ili kuomba Rushwa .

Waziri Maige amewataka askari hao kuepuka kutumia nguvu kwa kuwakamata wananchi na kuwa ofisi yake haitahusika na askari wanaoshindwa kufuata sheri a na kuwa wapo askari wanaochinjwa kutokana na unyama ambao wamekuwa wakiufanya kwa wananchi.

Chanzo: francisgodwin.blogspot

Friday, March 16, 2012

DAR ES SALAAM

WAKUU WA MIKOA MIPYA MINNE WATANGAZWA
Na Sandahillary Mnyawusuha
  • TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
     Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete,
    amewateua wafuatao kuwa Wakuu wa Mikoa .

    Dkt. Rajab Mtumwa Rutengwe ameteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa KATAVI . Kabla ya hapo Dkt. Rutengwe alikuwa Mkuu wa wilaya ya Mpanda.

    Ndugu Magalula Saidi Magagula ameteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa GEITA . Kabla ya hapo Ndugu MAGALULA alikuwa Mkuu wa wilaya ya Lindi.

    Ndugu Paschal Kulwa Mabiti ameteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa SIMIYU . Kabla ya hapo Ndugu MABITI alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Singida.

    Kapt. Asery Msangi ameteuliwa kuwa Mkuu wa
    Mkoa wa NJOMBE . Kabla ya hapo Kapt. MSANGI alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Iringa.

    Uteuzi huu unaanza tarehe 15 Machi, 2012 . Wataapishwa Ikulu, Dar es Salaam, Jumatano tarehe 21 Machi, 2012 saa 04:00 asubuhi .

    Imetolewa na : Kurugenzi ya Mawasiliano ya
    Rais, Ikulu . Dar es Salaam. 15 Machi, 2012

Tuesday, March 13, 2012

DAR ES SALAAM

KAMATI YA LIGI YAADHIBU WACHEZAJI 5 YANGA
Na: Sandahillary Mnyawusuha

Kamati ya Ligi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) iliyokutana Dar es Salaam jana (Machi 12 mwaka huu) imetoa adhabu kwa klabu mbalimbali na wachezaji sita wakiwemo watano wa Yanga.


Villa Squad imepigwa faini ya sh. 500,000 baada ya washabiki wake kufanya vurugu kwenye mechi namba 122 dhidi ya Azam iliyochezwa Februari 15 mwaka huu Uwanja wa Chamazi.


Pia klabu hiyo imepigwa faini ya sh. 300,000 kwa kuchelewa uwanjani kwenye mechi namba 129 dhidi ya Mtibwa Sugar iliyochezwa Februari 19 mwaka huu Uwanja wa Manungu. Adhabu hiyo ni kwa mujibu wa Kanuni ya 8(13) ya ligi hiyo.

Nayo Yanga imepigwa faini ya sh. 500,000 kutokana na washabiki wake kufanya vurugu kwenye mechi namba 132 dhidi ya Azam iliyochezwa Machi 10 mwaka huu. Pia klabu hiyo imepigwa faini ya sh. 500,000 kwa mujibu wa Kanuni ya 25(d) baada ya kuoneshwa kadi kuanzia tano kwenye mechi hiyo.


Mchezaji Juma Mohamed wa Polisi Dodoma amefungiwa mechi tatu na kupigwa faini ya sh. 500,000 baada ya kuwashambulia watazamaji kwa chupa ya maji katika mchezo namba 114 kati ya timu yake na Villa Squad uliochezwa Februari 11 mwaka huu.


Nadir Haroub ‘Cannavaro’ wa Yanga amefungiwa mechi sita za Ligi Kuu na kupigwa faini ya sh. 500,000 baada ya kuoneshwa kadi nyekundu kwa kosa la kumshambulia mwamuzi Israel Nkongo kwenye mechi hiyo namba 132.


Wachezaji wengine wa Yanga walioadhibiwa kutokana na mechi hiyo ni Nurdin Bakari amefungiwa mechi tatu na faini ya sh. 500,000, Omega Seme amefungiwa mechi tatu na faini ya sh. 500,000.

Jerryson Tegete amefungiwa miezi sita na faini ya sh. 500,000. Stephano Mwasika amefungiwa mwaka mmoja na faini ya sh. milioni moja kwa kumpiga mwamuzi Nkongo. Adhabu zote zimetolewa kwa mujibu wa Kanuni za Ligi Kuu.


Kamati ya Ligi imempongeza nahodha wa Yanga, Shadrack Nsajigwa na mshambuliaji wa timu hiyo Hamis Kiiza kwa kuwa mstari wa mbele kuzuia wenzao kumshambulia mwamuzi. Pia imempongeza kocha Kostadin Papic wa Yanga kwa kukemea vurugu zilizofanywa na wachezaji wake.

Saturday, March 10, 2012

DAR ES SALAAM

Madaktari wamtii JK, wasitisha mgomo rasmi

Kiongozi wa madaktari, Ulimboka

MADAKTARI nchini Tanzania wamesitisha mgomo wao mara moja ikiwa ni baada ya kufanya mazungumzo na Rais wa Tanzania, Jakaya Kikwete na kuwasilisha madai yao, huku akiahidi kuyafanyia kazi madai hayo.
Kwa mujibu wa taarifa ambayo mtandao huu umeipata kutoka kwa Jumuiya ya Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), imeeleza kuwa wamefikia hatua hiyo ya kusitisha mgomo baada ya kukutana na Rais Kikwete jana Ikulu.

Taarifa hiyo imesema kuwa Rais Kikwete amepokea hoja za madaktari na kuahidi kuzifanyia kazi. “Tulikutana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania MH. DR. JAKAYA MRISHO KIKWETE. Tulimweleza hoja zetu ambazo amezielewa na kuahidi kuzishughulikia kikamilifu. Tunaimani sana na MH. RAIS kwamba hatatuangusha.

“Kutokana na hilo tunapenda kuutangazia umma wa Watanzania kuwa tunarudi kazini rasmi kuanzia Machi 10, 2012, Wakati Mheshimiwa Rais akishughulikia madai yetu,” imesema taarifa hiyo ya MAT.

Hata hivyo katika taarifa hiyo MAT wameeleza wazi wazi kuwa hawana imani na WAZIRI WA AFYA MH. DR. HAJI MPONDA pamoja na Naibu wake MH. DR. LUCY NKYA, na kuwa wamemsimamisha uanachama wa MAT MH. DR. LUCY NKYA.

“Madaktari tunatamka wazi kuwa Waziri wa Afya DR. HAJI MPONDA na Naibu wake DR. LUCY NKYA ni maadui wa madaktari na sekta ya afya kwa ujumla hapa nchini na tunaahidi kutowapa ushirikiano wa aina yoyote wa kibinafsi au wa kiutendaji,” imesema taarifa hiyo.

Pamoja na kutoa tamko hilo pia MAT imetoa ufafanuzi juu ya mgomo wao ikisema kuwa;- kwanza Jamii ielewe kuwa daktari kama binadamu mwingine anayefanya kazi Tanzania ana mahitaji muhimu (basic needs) na mahitaji ya kijamii (social responsibility) na hivyo si chombo cha kufanyia kazi (Machine).
na pili, pia Daktari ana haki ya kupata ujira unaomfaa kutokana na kazi anayofanya na ana haki ya kuacha kazi muda wowote iwapo ataona kazi hiyo ya udaktari haimpi ujira wa kutosha na heshima ya kuendesha maisha yake.

Tatu, jamii itambue kuwa daktari anaweza kulazimishwa kurudi kazini lakini hawezi kulazimishwa kufanya kazi. Matokeo ya kulazimishwa yanaweza yasiwe mazuri kwa wale watakao hudumiwa na nne, jamii itambue kuwa madai na hoja kuu za madaktari ni kwa ajili ya faida ya Watanzania wote, yakiwemo mazingira bora ya kufanya kazi mjini na vijijini, na kuboresha afya za watanzania kwa ujumla. Pia vifaa na dawa ziwepo mahospitalini zinakohitajika.

Na mwisho MAT imewashukuru madaktari wote kwa mshikamano wetu tulioonyesha na tunaomba mshikamano huu uendelee daima.

Chanzo: the habari.com

Wednesday, March 7, 2012

DAR ES SALAAM

MADAKTARI MABINGWA MUHIMBILI NAO WAGOMA(GAZETI MWANANCHI)


Geofrey Nyang’oro na Florence Majani
WAKATI Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Jamii ikianza kazi ya kuzungumza na madaktari walio kwenye mgomo, madaktari bingwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) na walio katika Taasisi ya Mifupa (MOI) wamegoma. Mgomo huo wa jana ulihusisha vitengo vyote huku wagonjwa waliokuwa wamelazwa hospitalini hapo wakipewa taarifa za kuondoka katika wodi walimolazwa.

Azimio la mgomo huo lilifikiwa katika kikao cha dharura kilichoitishwa na jopo la madaktari bingwa wakiongozwa na Dk James Rwehabura ambaye ni daktari bingwa wa Kitengo cha Uchunguzi wa Magonjwa ya Binadamu.

Habari za ndani kutoka katika kikao cha dharura cha wanataaluma hao, zilisema uamuzi huo ulifikiwa kwenye kikao cha madaktari hao kilichoanza mapema asubuhi jana na kumalizika saa 6:00 mchana. “Kwa pamoja tumekubaliana kuweka vifaa chini, hii ni kutokana na ukweli kuwa hali ya utoaji huduma katika hospitali hii ni mbaya huku taarifa za Serikali zikiwa siyo za kweli,” alidokeza mmoja wa madaktari bingwa.

Daktari huyo aliyekataa kutaja jina lake, alisema, “Tumekubaliana kugoma hadi hapo Serikali itakapotoa majibu ya madai yote yaliyowasilishwa na jumuiya ya madaktari inayoongozwa na Dk Stephen Ulimboka kwa Serikali.” Jumuiya hiyo iliwasilisha madai mbalimbali likiwamo la kuitaka Serikali kupeleka vifaa na dawa katika hospitali za Serikali ili madaktari hao waweze kutoa huduma bora kwa jamii.

Pia, madaktari hao walitaka kusitisha safari za vigogo kwenda kutibiwa nje kwa magonjwa yanayotibika ndani kwa kile walichodai, hali hiyo inachangia wao kudharauliwa na pia kuzorotesha jitihada za Serikali katika uboreshaji wa mazingira ya kazi kwa madaktari hao.

Kwa nyakati tofauti, madaktari hao walibainisha sababu ya mgomo wao na kudai kuwa, kikubwa ni mazingira magumu ya kazi. Daktari mwingine ambaye hakupenda jina lake kuandikwa gazetini alisema, licha ya mishahara na posho ndogo, lakini mazingira ya kufanyia kazi yamekuwa magumu mno.

“Tumeshaamua , ‘tools down’ hospitali haina kitu, hata ‘mask’ hakuna badala yake tunavaa gozi tunapofanya upasuaji, acha hiyo, hata nyuzi za kushonea wakati wa upasuaji hakuna,” alisema daktari huyo. Daktari huyo alisema, hawawezi kufanya kazi katika mazingira hayo kwa sababu yatawasababisha kuwa na utendaji mbovu na baadaye taifa kuwalalamikia.

Alisema hapa nchini madaktari bingwa ni wachache, kwa hiyo kitendo cha wao kufanya kazi peke yao bila wasaidizi, yaani madaktari wa mafunzo na wale wanaomaliza, wanaelemewa na mzigo wa kazi. Dk Henry Mwakyoma, Mhadhiri Mkuu wa Chuo cha Udaktari Muhimbili, (MUHAS) ambaye hakuwapo katika kikao hicho cha dharura alidai kuwa, yeye kama mhadhiri hajagoma, lakini alikiri kuwapo kwa mazingira magumu ya kazi.

“Mpaka sasa hatujalipwa mishahara ya mwezi uliopita, halafu kazi yetu ndiyo kama hii tunatakiwa tufanye utafiti, unategemea tutafanya kazi kwa umakini kweli? Tutawafundisha madaktari kwa umakini?” alihoji Dk Mwakyoma.

Mwakyoma alisema, Serikali haiwezi kudai kuwa haina fedha za kutosha wakati imetumia mamilioni ya shilingi katika sherehe za miaka 50 ya Uhuru na uchaguzi wa Igunga. Alisema ni vyema Serikali ikajipanga na kuamua kushughulikia masuala ya madaktari kwa hekima kwani kukaa kimya bila kutoa suluhu ni sawa na kufanya ushindani usio na maana.

Hata hivyo, Ofisa Habari Mwandamizi wa MNH Aminael Aligaesha alisema jana jambo hilo lilikuwa likishughulikiwa kwani vipo vikao vinavyoendelea.

Wagonjwa watimuliwa wodini
Wodi mbalimbali hospitalini hapo zilitawaliwa na vilio kutokana na wagonjwa na ndugu za wagonjwa kupewa taarifa za kuondoka katika eneo hilo mara moja, kutokana na mgomo huo wa madaktari. Mmoja wa wagonjwa waliokuwa wamelazwa katika wodi ya Sewahaji, Sadick Dimoso (35) mkazi wa Morogoro alisema hali sasa MNH ni mbaya.

“Tumeambiwa tuondoke wodini bila ya kuruhusiwa na daktari, hii ni hatari tena wanasema tuondoke tukakae huku hadi wiki mbili ndio turudi kuangalia,” alisema Amina Ramadhani, aliyekuwa akisubiri kufanyiwa upasuaji wa jicho. Alisema hatua ya kutakiwa kuondoka hospitalini hapo imekatisha matarajio yao ya kuendelea kuwa hai na kuitaka Serikali kufanyia kazi madai ya madaktari.

Wakati kundi la watu wengine wakililia huduma hosptalini hapo, baadhi ya ndugu za wagonjwa waliingia katika mgogoro na walinzi wa wodi hiyo ya Sewahaji wakitaka waandishi wa habari kuingia wodini.

Vikao vya Kamati Wakati hayo yakijiri, vikao baina ya madaktari na Kamati ya Kudumu ya Huduma za Bunge, viliendelea jana katika ofisi ndogo za Bunge huku taarifa zake zikiwa ni siri.www.mwananchi.co.tz 
Chanzo: mjengwa.blogspot.com

Tuesday, March 6, 2012

NJOMBE


WANAFUNZI WAFANYA MAANDAMANO
Na Kalmas Konzo

Zaidi ya wanafunzi 1000 wa shule za msingi Mpechi na Sabasaba wakiongozana na baadhi ya walimu wa shule hizo pamoja na wazazi wengine walifunga barabara kuu ya Njombe - Songea kwa zaidi ya masaa matatu wakiishinikiza serikali kujenga matuta katika barabara hiyo kwa lengo la kudhibiti ajali za mara kwa mara zinazotokea katika barabara hiyo.

sakata hilo lilianza mara tu baada ya wanafunzi kupata taarifa ya kifo cha mtoto Irene Kadege aliyekuwa akisoma darasa la awali katika shule ya msingi Sabasaba.

Kifo cha mtoto huyo kilitokana na kugongwa na gari lenye namba za usajili T 612 AQP jirani na ofisi za TANESCO Njombe.

Wanafunzi hao waliifunga barabara hiyo huku wakiandamana kutoka maeneo ya shule zao mpaka maeneo ya stendi kuu huku wakiimba nyimbo za kuhamasisha madereva wawe makini wanapoendesha vyombo vya usafiri barabarani.

Hali hiyo ya mtafaruku wa wanafunzi ilikuja kutulizwa na mkuu wa wilaya ya Njombe Mh. saraha Dumba ambaye aliwaahidi wanafunzi hao kwamba suala la kujenga matuta mapema iwezekanavyo ikiwa ni sambaba na kuwaweka askari wa usalama barabarani katika eneo hilo ambao watahakikisha usalama wa waenda kwa miguu.

Kumekuwa na ongezeko la ajali za barabarani katika barabara ya Njombe - Songea hali inayosababishwa na madereva wazembe wanaoshindwa kuzingatia sheria za usalama barabarani.

Sunday, March 4, 2012

SIMBA YAIFUNGA TIMU YA KIYOVU YA RWANDA 2-1

Mchezaji wa timu ya Simba mganda Emmanuel Okwi kulia akijaribi kumtoka mchezaji wa timu ya Kiyovu ya Rwanda wakati wa mchezo wa Kombe la Shirikisho katika ya timu hiyo na Kiyovu ya Rwanda unaofanyika kwenye uwanja wa Taifa jioni hii.
Simba imefanikiwa kuiondosha Kiyovu ya Rwanda magoli 2-1, magoli ya Simba yamepatikana katika kipindi cha kwanza na yamefungwa na mshambuliaji Felix Sunzu akipokea pasi nzuri, kazi iliyofanywa na mchezaji Emmanuel Okwi wa Simba. Timu ya Kiyovu imefanikiwa kupata goli lake la kwanza katika kipindi cha pili cha mchezo huo, hata, Simba imefanikiwa kusonga mbele katika mashindano hayo ya Kombe la Shirikisho barani Afrika,
Wachezaji wa timu ya Simba Emmanuel Okwi na Felix Sunzu wakishangili mara baada ya mchezaji Felix Sunzu kufunga goli la pili kati ya magoli mawili aliyofunga
Timu zikiingia uwanjani kabla ya kuanza kwa mchezo huo jioni hii.
Mashabiki wa Simba wakishangilia kwelikweli wakati timu hizo zikicheza.
Kulikuwa n a kila shamrashamra kwa mashabiki wa Simba kama unavyowaona katika picha.
Hii inaashiria kwamba kama matokeo yatakuwa hivihivi mana yake ni kwamba Simba itaendelea kukwea Mwewe yaani Ndege kwa ajili ya kushiriki raundi ya pili ya michuano hiyo.
Chanzo: mjengwa.blogspot

Saturday, March 3, 2012

CHAMA CHA MAPINDUZI (CCM) CHAMTANGAZA SIYOI SUMARI KUWA MGOMBEA WAKE ARUMERU


Kamati kuu ya chama cha mapinduzi (CCM) iliyokuwa imeketi leo imemaliza kikao chake jioni hii na kumtangaza rasimi aliyeshinda kura za maoni Bw Siyoi Sumari kuwa mgombea wa ubunge wa jimbo la Arumeru Mashariki kusaidia kutetea jimbo hilo dhidi ya vyama vya upinzani.

Taarifa zilizotua hivi punde katika mtandao huu kupitia studio za radio uhuru zinadai kuwa kutangazwa kwa mgombea huyo ni mwanzo wa CCM kuingia katika kinyang'anyiro hicho

Chanzo: francisgodwin.blogspot

Thursday, March 1, 2012

IRINGA

MAKAMU WA RAIS DR. BILAL ASHUHUDIA NGUVU YA CHADEMA JIMBO LA IRINGA MJINI

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akiagana na Mbunge wa Jimbo la Iringa mjini, kupitia tiketi ya CHADEMA, Mchungaji Peter Msigwa, wakati akiwa Uwanja wa Ndege wa mkoani Iringa jana akirejea jijini Dar es Salaam baada ya kumaliza ziara yake ya mkoani humo. Picha na Muhidin Sufiani-OMR
MAKAMU wa Rais Dk Mohamed Gharib Bilala ashuhudia kifo cha chama cha mapinduzi (CCM) jimbo la Iringa mjini baada ya chama cha Demokrasia na maendeleo (chadema) wilaya ya Iringa mjini kuwataka wafuasi wa chama hicho walioshiriki mkutano wa hadhara wa makamu huyo wa Rais kuonyesha itikadi yao dhidi ya Chadema.

Makamu wa Rais alishuhudia nguvu hiyo ya chadema baada ya mwenyekiti wa Chadema wilaya ya Iringa mjini na mbunge wa jimbo la Iringa mjini mchungaji Peter Msigwa kutumia jukwaa hilo la Makamu wa Rais kukionya chama cha mapinduzi (CCM) mkoa wa Iringa kwa kujimilikisha ziara za viongozi wa serikali kwa kuweka bendera za CCM na kujipigia debe .

" Mheshimiwa makamu wa Rais naomba leo nitoe onyo kwa CCM na kuwaonyesha kuwa si vizuri kuteka misafara ya viongozi wa kitaifa wa serikali wanapokuwa katika ziara mkoani hapa...imekuwa ni kawaida ya CCM kutumia majukwaa haya kujipigia debe sasa naomba uniruhusu kuwasalimu wananchi kwa falsafa ya chama changu cha Chadema .....naomba wananchi wote kunjeni ngumi nikisema peoples semeni Power’ " salamu hiyo ilifanya robo tatu ya wananchi waliojitokeza katika mkutano huo uliofanyika uwanja wa Mwembetogwa juzi kulipula kwa sauti kubwa na kujibu salamu hiyo 

Hatua ya mbunge Msigwa kumwonyesha makamu wa Rais nguvu ya Chadema ilitokana na na Mkuu wa Wilaya ya Iringa,Kapt. Mstaafu Asseri Msangi kumtaka kupanda jukwaani ili awasalimu wananchi wa Manispaa hiyo kama ilivyokuwa kwa wabunge wa CCM

Baada ya salaam hizo mbunge huyo alimweleza Makamu wa Rais na ujumbe wake kwamba kwa kuwa na yeye (Msigwa) ni Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Iringa, angeamua kuwaambia wananchi wake wabebe bendera zao au kuvalia kombati za chama chake ingekuwa balaa.

“Kama na mimi ningewatuma wananchi wangu wabebe bendera au kuvalia mavazi ya chama (Kombati) ingekuwa balaa lakini naomba niwasalimu wananchi wangu kwa salaamu ya chama chetu…’Iringa, Peoplesssss,wananchi wakaitika Power! huku wakinyoosha vidole viwili juu jambo ambalo lilimlazimu Msigwa kuwaambia wananchi hao, nawaombeni sasa, mumsikilize mheshimiwa Makamu wa Rais,”alisema mbunge huyo.

Hata hivyo CCM kupitia katibu wake wa mkoa Mary Tesha alipanda jukwaani na kutaka kujaribu kuonyesha nguvu ya CCM kwa kusalimia kwa salamu ya CCM na kujibiwa na watu wasio zidi 50 wakiwemo viongozi wa jukwaa kuu huku watu zaidi ya 10000 wakinyamaza kimya na kuzomea .

“CCM Oyeee! Mheshimiwa Makamu wa Rais siyo kweli kwamba tumekuwa tukiteka ziara wala kuipora mikutano ya serikali kwa kuweka bendera zetu.
Hata mheshimiwa mbunge (Msigwa) anajua kwamba Makamu wa Rais amekuja kukagua miradi inayotekelezwa kwa ilani ya CCM,”alisema katibu huyo akijibu kauli iliyotolewa na mbunge wa Iringa mjini (Chadema).

Hata hivyo,katika hali isiyo ya kawaida wakati mbunge huyo akitumia salaam ya Peoples Power, Dk.Bilali alikuwa mtulivu na hakuonekana kuvurugwa na falsafa hiyo hata wakati alipopanda jukwaani kuwahutubia wananchi wa Manispaa ya Iringa waliofika kumsikiliza.

Mbali ya Chadema kuchukizwa na utaratibu huo wa CCM kupeperusha bendera za CCM katika uwanja huo bado Chadema ililazimika kupamba bendera zake kando kando ya barabara ya Kihesa na wakati msafara wa makamu wa Rais uliokuwa na magari zaidi ya 40 ukipita katika eneo hilo kuelekea uwanja wa ndege Nduli ulishuhudia utitiri wa bendera hizo za Chadema .

Chanzo: francisgodwin.blogspot.com